Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba Zanzibar, Bi.Mwanaisha Alli Said, amefanya ziara ya kikazi Pemba kwa kutembelea Ofisi kuu ya Shirika la Nyumba iliopo mjini Chakechake.
Katika ziara hio amekutana na Watendaji wakuu na wafanyakazi wa Ofisi hio kwa lengo la kujitambulisha na kuzungumzia mikakati ya utekelezaji kazi ya Shirika kwa upande wa Pemba na changamoto zinazolikabili Shirika. Vilevile amejadili hatua mbali mbali za kutatua changamoto hizo ili kuboresha utendaji kazi, ili Shirika liweze kupiga hatua zaidi.
Vile vile, Mkurugenzi alifanya majadiliano juu ya majukumu ya wafanyakazi hao na kusikiliza changamoto zinazowakabili. Pia aliwasihi wafanyakazi hao kufanya kazi kwa weledi, uaminifu na kushirikiana nae kwenye kuleta maendeleo kwenye Shirika kwa kupunguza matumizi yasiyo ya lazima. Pia, aliwasihi wafanyakazi hao kubuni mbinu mpya za kuwahamasisha wapangaji kulipa kodi kwa wakati ili Shirika lipate pato zaidi la kuweka kwenye Uwekezaji wa ujenzi wa nyumba nyingi zaid ili liweze kuwapatia wananchi makaazi bora pamoja na kuzifanyia ukarabati nyumba zilizopo chini ya Shirika.
Wakati huo huo Bi. Mwanaisha alifanya ziara kwenye Nyumba mbalimbali za Shirika zikiwemo Nyumba za Maendeleo za Madungu, Nyumba za Maendeleo za Machomane, Jaani Building, pamoja na kwenda kuona ujenzi wa Septic Tank (Karo) iliopo Tibirinzi.