Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makaazi Zanzibar na Shelter Afrique kwa kushirikiana na Shirika la Nyumba Zanzibar imefanya mkutano wa Wadau, kwa lengo la kujifunza na kujadili fursa mbalimbali za ujenzi wa Nyumba za bei nafuu (Affordable Housing). Mkutano huo ulifanyika hoteli ya Golden Tulip Airport Zanzibar.
Katika mkutano huo mgeni rasmi alikua Waziri wa Ardhi na Maendeleo ya Makaazi Zanzibar, Mhe. Riziki Pembe Juma ambae alielezea malengo ya serikali katika kufanikisha azma hiyo ya kuwapatia Wazanzibari nyumba bora na za gharama nafuu.
Aidha, Viongozi mbali mbali wa Serikali pamoja na wadau kutoka Taasisi za Serikali na Sekta Binafsi walihudhuria na kutoa michango yao na maoni juu ya kufanikisha jambo hilo.
Miongoni mwa mambo yaliyojadiliwa ni pamoja na fursa ya Ujenzi wa Nyumba za Bei Nafuu na jinsi Serikali ilivyojipanga kutumia fursa hio katika kuleta maendeleo ya makaazi bora na salama
Zanzibar ili kukidhi mahitaji ya makaazi ya Wananchi ambayo yanaongezeka kila siku.